Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba leo amepongeza jitihada zinazofanywa na Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) za kutembelea miradi mbalimbali inayotekelezwa katika Mkoa huo ikiwa ni  sehemu ya Mafunzo ya wanachuo hao ili kuona, changamoto na mafanikio mbalimbali  katika miradi hiyo.

Pongezi hizo amezitoa leo katika ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa alipokutana na viongozi na wanafunzi wa chuo hicho ambao watatumia wiki moja kutembelea kiwanda cha kuchakata pamba, vikundi vya vijana, migodi mbalimbali ya madini na baadhi ya mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali.

Akitoa taarifa ya awali kuhusu maendeleo ya Mkoa huo RC Serukamba amewaeleza kwamba 

Mkoa umeongeza eneo la kilimo kupitia wakulima wadogo na wakubwa kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa Alizeti ambapo inatarajiwa kuvunwa kwa wingi msimu huu.

Aidha Serukamba akijibu swali la Mwanafunzi mmojawapo katika ziara hiyo ya Wanachuo aliyetaka kujua kama kuna migogoro ya wakulima na wafugaji na namna inavyotatuliwa ambapo RC Serukamba ameeleza kwamba Mkoa unatekeleza mipango ya matumizi Bora ya ardhi na wameimarisha ufuatiliaji wa karibu unaofanywa na viongozi wa Kata na Tarafa ambayo imesaidia kupunguza migogoro hiyo.

 Hata hivyo RC Serukamba amekiri kwamba ziara hiyo itasaidia kuleta chachu kwa watendaji katika kuimarisha usimamizi na ufuatiliaji wa kazi za Serikali kwa weledi.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo hicho Meja General Ibrahimu Michael Mhona amesema ziara yao Mkoa wa Singida ni ya wiki moja katika Wilaya za Singida Mkalama Ikungi Itigi na Manyoni na italeta matokea makubwa kwa kuwa taarifa hizo zinatumika katika kuwashauri viongozi mbalimbali.

Ameendelea kueleza kwamba ziara hiyo ambayo inatekelezwa kwa nchi nzima ambapo wamegawana makundi mbalimbali ambayo yanakagua mambo ya usalama, uchumi, kilimo na mambo mbalimbali ya kijamii.


Post a Comment

 
Top